NAPOA YAWAASA WAZAZI KUWALEA NA KUWAFUNDISHA WATOTO MAADILI MEMA.

 


NAPOA yawaasa wazazi kuwalea na   kuwafundisha watoto maadili mema. 

Na Ahmad Mmow, Nachingwea.

KUTOKANA na ongezeko la  vitendo vya ukatili wa kijinsia wilayani  Nachingwea mkoa wa  Lindi, shirika lisilo la kiserikali la Nachingwea Paralegal Aid Organization (NAPAO) limeamua kutoa elimu ya sheria ya mtoto. Ambapo leo tarehe 17.06.2024 limetoa elimu hiyo kwa wananchi wa kijiji cha Mkonjela Chini ili jamii itambue haki za watoto na wajibu wao katika malezi.

Akizungumza na wananchi hao kuelekea siku ya mtoto wa Afrika. Mkurugenzi wa Shirika hilo ambalo sio la  kiserekali ambaye pia ni msaidizi wa kisheria,Sabrina Dossa alisema wazazi lazima watambue haki za watoto kama vile kuwapa ulinzi,elimu na  mahitaji yote muhimu.

 Alisema wazazi wanapaswa kufichua matendo yote ya ukatili wa kijinsia,kama vile ulawiti, ubakaji na ndoa za utotoni ili kuwa na kizazi bora kwa faida ya familia na taifa kwa ujumla.

Alitoa wito kwa wazazi ,walezi na jamii  kuwa makini katika malezi kwa kuwafunza watoto mila na tamaduni zao na  kuwapatia mafundisho yenye maadili mema  kwa jamii na maisha yao kwa ujumla.

Kwa upande wake ofisa habari na mawasiliano wa shirika hilo, Christopher Lilai alisema kuwa shirika linatoa msaada wa kisheria,ushauri wa kisheria kwa jamii,  na usuluhishaji wa migogoro  kwa wananchi  ambao hawana  uwezo wa kifedha wa kugharamia.

"Shirika letu linatoa huduma  za kisheria   bila malipo yeyote  kwa wale ambao hawana uwezo lengo ni  kumfanya mwananchi  apate haki yake bila kuathiriwa na umaskini"alisema Lilai.

Nae alitoa wito  kwa kila mwananchi anae hitaji msaada huo  aende katika ofisi za shirika hilo au kwa wasaidizi wa kisheria waliopo kwenye kata 14  zilizopo ndani ya wilaya ya Nachingwea.

Mmoja wa wazazi wa kijijini hapo,  Zuhura Ungele alisema kwamba, baaadhi ya wazazi wanawagopa watoto wao wanaosoma  sekondari hivyo kusababisha watoto wengi kuwadharau wazazi wao baada ya kufika kidato cha nne  na kuendelea. Kwani wanajiona  ni wasomi kuliko wazazi wao.

Mwananchi huyo alisema  mwenendo wa maisha ya watoto  sio mzuri. Kwani asilimia kubwa yanakiuka maadili ya watanzania. Hivyo alitoa wito  kwa watoto wote kuanza kuwajibika kwa wazazi wao ili wapate malezi bora na mema.

Post a Comment

0 Comments